Saturday, August 21, 2010

WOSIA KWA WAHITIMU WA 2010 KISARE NURSING SCHOOL

Vitabu katika Maktaba ya Kisare Nursing School
Wapendwa Wahitimu,
Kisare Nursing School,
Mugumu, Serengerti,

Sanjari na kuwatunuku Wahitimu vyeti husika, mara nyingi inapofika siku ya mahafali mengi yanasemwa na kuimbwa katika ama kuwapongeza au kuwahasa kama siyo kuwaangaliza katika majukumu yatakayowakabili katika jamii.

Turuhusuni nasi leo tuwatunuku nukuu chache zinazohusika na KUPATA ELIMU kama tafakuri mtakazozibeba katika fikra zenu kama zilivyoanikwa na magwiji katika nyanja na tasnia mbalimbali kama ifuatavyo:-

 “Vitabu vyaweza kuwa hatari, vile vyenye uzuri wa hali ya juu, ni vema vikawekewa tahadhari isemayo, Onyo, hiki kinaweza kubadilisha maisha yako”. Helen Exley .


 “Vitabu na maandiko yote ni tishio kwa wale wanaonuia kuiminya kweli.”
Wole Soyinka.


 “Upo utofauti kati ya mwenye ari atafutaye kusoma kitabu na asiye na ari atafutaye kitabu cha kusoma”. Gilbert Chesterton


 “Kusoma ni nauli yenye unafuu kuelekea kokote”. Mary Schmich.


 “Elimu yetu inatakiwa kutupa chanjo ya kujituma kwa ajili ya jamii nzima na kuwasaidia wanafunzi kukubali yale yanayokubalika kwa ajili ya maisha yetu ya mbeleni”. Baba wa Taifa, Mwl. J. K. Nyerere


 “Elimu ni siraha ya nguvu kubwa unayoweza kutumia kuibadili dunia”. Nelson Mandela.


 “Mizizi ya elimu ni michungu, lakini matunda yake ni matamu”. Aristotle.


 “Wakati mnaondoka hapa (Chuoni), msisahau kwa nini mlikuja hapa”. Adlai Stevenson








Masomo yenu hapa yanaweza kuwa yamefika ukingoni,
lakini kumbukeni kuwa kuelimika kunaendelea daima!
Wahitimu, Wakufunzi, Watumishi na Wadau wengine wote
hongereni sana na tunawatakieni kila la kheri.


Wenu,

Judy, Marja & Musuto Chirangi
Uholanzi, July, 2010.

No comments: