Thursday, January 3, 2008

SHUHUDA, MAONI NA USHAURI WA WAGENI WA A.M.CHIRANGI



Kutoka Kushoto (Mwenye kitambaa Cheupe) Mjane wa Mzee Mutaragara, mama Bertha Nyabwire na mjukuu wake Judith na kulia ni Bibi (Marehemu) Nyarukonge Mjane wa Babu Faru wa Muhongo watu waliomlea mzee Mutaragara.
------------------------------

Yafuatayo ni mawazo ya sehemu ndogo tu ya wageni wenye demografia mbalimbali waliokuwa wakimtembelea mzee Chirangi maana alipenda sana kukaribisha wageni. Kama ilivyo kiada, Mzee Chirangi aliwapa namba na kisha kitabu kwa ajili ya kuandika maoni au mawazo yao ambayo aliyatunza.

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba.116.
ASkofu S. B. M. Muttani
Kamunyonge Area, S.L.P. 336, Musoma
11/07/1996.

MAELEZO:
Ndugu A.M. Chirangi,
Mwenyekiti wa CCM,
Musoma – Mjini.

KAZI YA USHUJAA KWANGWA PLOTS.

Ndugu Mwenyekiti, Suala hili juu, siyo lelemama.

Kutokana na kauli yako yenye moyo safi, kunizungumza mara nyingi; ili nitembelee eneo la Kwangwa.

Kwa hiyo, asubuhi ya tarehe 11/7/1996, nilipanda Baiskeli yangu mpaka kwenye eneo lenyewe, ambalo limeanzia katika bonde la Kigera hadi uwanda wa Kwangwa.

Wahenga walinena muungwana ni kitendo, kuhusu usemi huu. Wewe mwenyewe umetekeleza kwa kitendo halisi; ambacho kinaonekana kwa Mungu na kwa watu sawia.

Kwanza, hulipata dhana nadharia, kuwe na sehemu ya makazi ya watu.

Pili, ukaangaika kutoa ushauri kwa wakaaji wa Kwangwa wakubali kuacha viwanja vyao, viwe makazi ya Umma.

Tatu, ukasimamia wewe mwenyewe kwa hali na mali kwa muda wote, wa kufyeka machaka na kuziba korongo na upashaji wa miamba na mawe n.k.

Nne, kusimamia uchoraji na upimaji wa viwanja na barabara, kwa utaalamu sahihi.

Tano, kuelekeza kwa kuzingatia hulka za jamii yaani kutenga maeneo ya utamaduni wa jamii.

Hivyo ukaweka viwanja vya burudani k.v. Makanisa, Misikiti, Shule, Chekechea na Soko n.k.

Sita, ilibidi upige mbiu kwa wananchi, ili wajipatie viwanja vya kujenga nyumba zilizo na hakika, sasa na baadaye bila migogoro.

Saba, kwa uthabiti wa fadhila yako ya moyo wa ushujaa, umekuwa mstari wa mbele kufyeka vichaka na kung’oa mawe. Hatimaye kujenga makao ya hakika, “Hongera sana”.

Umeweka alama kwa Ramani katika historia ya vizazi vifuatavyo.

Baada ya kisa, mkasa, usemi huu umenihulkisha kuwa na mkasa, kuomba usaidie kupata viwanja viwili ambavyo vitakuwa karibu na mto Kigera Magharibi.

Tamati, ujira wa nguvu zako hutalipwa hapa duniani na baadaye huko peponi.

Kwa hiyo, tukimwinulia Bwana macho ya mioyo yetu. Yeye amejaa fadhili nyingi.

Maana ndiye amlipaye kila mtu sawasawa na haki yale (Zab. 62:12).

“Yeye azidi sisi tupungue”
**************************************






Mzee Mutaragara na familia yake pamoja na wakweze

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 166.
Vivian Juma- Mwenyekiti wa Mkoa (CHADEMA) na
Mmratibu Kitengo cha Wanawake Taifa (CHADEMA)
BOX 1482, Musoma.
07/01/1999

MAELEZO:
Natoa shukrani kwa wema wako Mheshimiwa Mutaragara Chirangi na ni histori kubwa kwani sijawahi kukaribishwa hasa na heshima ambayo nimepewa ikibainika kwamba mimi ni kiongozi wa upinzani. Hivyo ni heshima ambayo sitaweza kuisahau siku hii ya leo.

Mungu abariki nyumba hii.

****************************************

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba . 228.
Mh. H. Hepillal N. Ole – Molloimet – Mkuu wa Wilaya Musoma
P.O. BOX 20, Musoma
Aug. 2001

MAELEZO:

Mimi na ujumbe wangu kutoka Wilayani nimefurahishwa sana na makaribisho yako nyumbani kwako - hatimaye katika makazi yako ya baadaye, mapya Kwangwa ambako tumeweza kuona jitihada zako za hali ya juu, mipango ya sasa na baadaye, utundu na utashi wako katika kubuni mambo ya sasa na baadaye, mipangilio ya uwekaji kumbukumbu zako za maisha, mali, vifaa, taarifa mbalimbali za uongozi wako, jambo ambalo hata baadhi ya watu hawafanyi. Busara zako, utu wako na hekima zako ni hazina kubwa sana sio kwa familia yako tu bali kwetu sisi
sote. Umetufundisha umetuonyesha na kutuelekeza tulivyo na ulivyo wewe ni mtu wa kuigwa na wale wasio na choyo! Wewe ni kero kwa wale wasiopenda haki, uwazi na ukweli na haki. Wewe ni mtu wa watu wakati wa uongozi wako na hata sasa ndani ya jamii wewe ni mfano wa kuigwa na wale wasio na choyo.
Mimi ni mmoja akutakiaye mema na familia yako na kukutakia maisha marefu pesa na wakati ujao. Endelea na moyo huo usikate tamaa kwani kufanya hivyo ni dhambi – dawa ni kujua. Kwako, wewe, wanao, wajukuu, vilembwe na vilembwekezo – muwe na rutuba ndani ya jamii.
************************************************










Mzee Mutaragara aki'pozi' kwa ajili ya picha na familia yake.
UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 265.
Dr. Mwitondi Kassim Saidi (Ph.D)
School of Mathematics
Universty of Leeds
United Kingdom
07/02/2004

MAELEZO:

FACE TO FACE WITH MUTARAGARA CHIRANGI.

I knew Mzee Chirangi as a dedicated school teachers, social worker and active sports activist. The past was particularly interesting as it went down well with my personal interest namely watching and playing football, little did I know then that almost 30 years later I would be brought to face with Mzee Chirangi in a surprise encounter that would unfold a lot of facts about him, his human, moral and social properties as I had never anticipated. This is how I got to talk to Mzee Chirangi. I had just returned to Musoma from the United Kingdom, for the funeral of my father – Mzee Said Mwitondi who passed away on the 4th of February 2004, barely a week after I had parted with him to return to the UK.
Living within the area, Mzee Chirangi had decided to pop in and pass his condolences. This by itself is a wonderful moral property as Mzee Chirangi never knew our family but felt a moral obligation to pay us a visit at that difficult moment but like a shimming star in the sky everyone in our family knew him – not least myself, as I had earlier tried to get some sporting information through him. I had contacted Professor Sospeter Muhongo, my former teacher, friend and adored football player, who in turn introduced me (by email) to Musuto Chirangi the son of Mzee Chirangi. For some reasons, the sought information could not be obtained for over 3 years. Believe me what I could not get in 3 years, I got with a couple of hours meeting Mzee Chirangi. The required information was on football activities in Musoma in particular, photographs of the guardians and players of the 70 who characterised Musoma footballing boom in my teenage. I needed then for a Musoma website, the link to which is available from my official website below. So when Mzee Chirangi visited us my immediate request to him was about this long-overdue plan and he immediately invited me (with two other friends) to visit him at his Kamunyonge residence. In the light of that invitation – I started laying down the strategies of comparing my theoretical knowledge of Mzee Chirangi with the ‘empirical readily’.
We arrived at Mzee Chirangi’s residence about 7.15 pm on 7th February, 2004.
Less than 30 minutes later I was up dating my knowledge of Mzee Chirangi with a new property of a “LIVING ARCHIVE”. He took us through massive archive files ranging from education, sports, social services and spirituality manual databases so informative that one of my friends suggested that Mzee Chirangi liaise with the relevant ministries to put the data to even better use. Another newly acquired piece of information was that Mzee Chirangi was a “Politician with a different attitude”. In Tanzanian political terms a typical politician is associated with some level of corruption (you are welcome to your own views if you disagree). Listening to the way Mzee Chirangi spoke, browsing through his writings, speeches and vision, left no doubt that he was what most “typical politicians aren’t”. Look at the following contesting cases. One works on individual’s voluntary service in a local neighborhood (and charges nothing) while another individual does the same and quotes an ample of million shillings. The former is Mzee Chirangi, working at Kwangwa, Kigera and Kiara and the letter is an “Unknown” individual channeling quotations through the Town Council.
Family is also an important entity in Mr. Chirangi’s life (you may argue that it is in every one’s life). Daily routine is clearly laid down as are basic principles that guide human life. My recommendation is for Mzee Chirangi to put his work in a more formalized style books/ CD ROM and be officially archived for the benefit of generations. I will be happy to assist into that direction.
*****************************
Mzee Mutaragara kama ilivyokuwa kawaida yake alikuwa akiendaButiama kwa rafiki yake baba wa Taifa J.K.Nyerere mara kwa mara. Hapo ameambatana na Mdogo wake Prof. Muhongo, Mkewe na wanawe.

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 277.
Rashon M. Matete, Mwenyekiti wa Wazazi – Musoma Mjini.

MAELEZO:
Maelezo yangu kimuhtasri yahusuyo Mzee A. M. Chirangi ni kama ifuatavyo:-
Alipokuwa mwalimu wakati wa shule za serikali na madhehebu alidhihirisha uwezo wake wa kufundisha hasa alipokuwa anafundisha darasa la nne wakati huo. Shule zote za Primary I – IV alizopata kufundisha katika dhehebu la TMC zilikuwa mfano mzuri katika Jimbo la Ziwa Wilaya ya Musoma.

Mzee A. M. Chirangi alikuwa mwalimu darasani, wanafunzi wake wa darasa la nne walifaulu kwa wingi kuingia katika shule za kati (Middle School)
Kwa kujiweka katika uhodari huo hatimaye aliteuliwa na dhehebu hilo la TMC kuwa Katibu wa Elimu wa TMC. (Education Secretary) na Primary Schools I - IV.

Hii ni picha kamili inayodhihirisha kwamba juhudi zake za kutoa huduma kwa wanadamu hazikuanza jana. Ni tangu ujana hadi uzee.

Juhudi mbalimbali za kuwasaidia wananchi wa Musoma na Mkoa wa Mara kwa ujumla zilizidi kujitokeza kwa kiwango kikubwa alipochaguliwa na wana C.C.M. kuwa Mwenyekiti wa C.C.M. Wilaya ya Musoma Mjini na pale alipokuwa Mwenyekiti wa Jumiya ya Wafanyakazi.

Kwa hiyo mimi binafsi ninaelewa kuwa Mzee A. M. Chirangi ana haya ya kuiga na yanayompa sifa nzuri:-
- Mchapa kazi tangu ujana wake mpaka sasa.
- Ana uzoefu katika uongozi na uendeshaji.
- Anafaa sana katika ushauri nasaha unaohitajika kwa watu walio wengi.
- Ni mfano pekee wa dhati kwa nchi yake na watanzania wenzake.
- Amejitahidi kujiweka katika mazingira ya kusaidia jamii na taasisi mbalimbali kuelewa mbinu za kupambana na mazingira yao.
- Ni mtu ambaye yuko miongoni mwa watu ambao waliombea Taifa hili Amani.
- Ni mtu ambaye anataja kosa waziwazi bila woga.
- Ni mpenda haki na msema kweli pindi suala kati ya mtu na mtu ua miongoni mwa watu linapojitokeza.
- Ni mtu anayetunza akadi na muda kwa jambo hili yeye ni pekee katika mji huu wa Musoma.
- Ni mbunifu wa kuigwa anapopewa madaraka.
Kwa hahika siwezi kutaja mambo yote yanayomhusu Mzee huyu bali ninachomalizia kusema ni kwamba ni vema kuiga mazuri ambayo Mzee A. M. Chirangi amefanya katika maisha yake ili iwe faida kwa vizazi vijavyo.

Mungu wetu wa mbinguni ampe baraka na maisha marefu kwa madhumuni ya kukamilisha mradi wake wa ujenzi wa mji mpya huko Kiara.
**********************************************










Mzee Mutaragara akiwa nyumbani kwao Kawawa st. Musoma wakati wa chakula cha pamoja na mazungumzo pamoja na Mkewe, Shangazi yake, Mdogo wake (na mkewe) na Dada zake.

UTAMBULISHO WA MGENI:

Namba. 305.

EMMANUEL MULESI
RADIO VICTORIA FM.
29/01/2006.

MAELEZO:
Nilifika nyumbani kwa Mzee Mutaragara Chirangi, kwenye majira ya saa 10 jioni, Tarehe 29/01/2006 eneo la Kwangwa.

Katika safari hii nikiwa njiani nilijionea mambo mengi ambayo pia nilijifunza vitu vingi sana kutoka kwa Mzee huyu.

Mambo makubwa niliyoyaona ni pamoja na jitihada kubwa ya Mzee huyu kujituma na kujitolea katika kuleta maendeleo hasa katika kuleta maendeleo katika maeneo ya Kigera na Kwangwa, hasa katika sekta za barabara na maji.

Nilijionea zaidi ya barabara 20 ambazo amejitolea kuzijenga kwa nguvu zake mwenyewe, pamoja na kuweka bomba kubwa la maji kwa maeneo hayo.

Mambo hayo yalinishtua kidogo kabla ya hata kufika nyumbani kwake Kwangwa.

Tulipofika nyumbani hapo nilizidi kustaajabu kujionea nyumba ya Mzee Mutaragara ambayo alianza kuijenga mwaka 1994, kwa kweli ujenzi wa nyumba hiyo ilinionyesha ni kwa jinsi gani Mzee huyu alivyo mkarimu, kutokana na ujenzi wa nyumba yake kuzingatia sehemu mbalimbali ambazo ameziandaa kwa ajili ya wageni wanaokuja kumtembelea kupumzika.

Pia ujenzi wa nyumba hiyo unaonyesha ni kwa jinsi gani amejiandaa kwa maisha yake bila kuwa na shida ya maji katika nyumba hiyo na pia utunzaji wa mazingira.

Nilipoingia ndani ya nyumba hii ya Mzee Mutaragara ndipo nilipothibitisha kuwa Mzee huyu ni mtu ambaye anatunza kumbukumbu zake kwa kila kitu anachokifanya katika maisha yake ya kila siku, na anaonekana ni mtu anayejali muda kwa kujiwekea ratiba yake ya kila siku, na anaonekana ni mtu anayejali muda kwa kujiwekea ratiba yake ya kila siku tangu kuamka mpaka wakati wa kulala.

Mbali ya hayo niliyoyaona na kujifunza kuwa Mzee Mutaragara ni mtu mwenye KIPAWA cha uongozi na ni mtu mwenye MAONO na uongozi kutokana na kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi kwa miaka mingi iliyopita.

Nimejifunza kuwa siri kubwa ya uongozi wa Mzee Mutaragara Chirangi ni
HEKIMA na BUSARA, katika kuwaongoza watu mbalimbali.

Nilipomuuliza siri ya yeye kuongoza kwa muda mrefu ni ipi? Alinijibu kuwa mara nyingi yeye amekuwa akifanya kazi bila ya kujali mkubwa, mdogo, jinsia, rangi, maskini au tajiri na pia yeye mara nyingi huwa na maono ya kuangalia mbele na kuona kuna nini? Ambacho kinaweza kujitokeza na kukitatua kabla hakijatokea na kuleta matatizo.

Pia katika ziara hii nimeona kuwa Mzee Mutaragara ni mtu mwenye uwezo wa kuelewa na ni kiongozi shujaa katika kufanikisha mambo yake ya ongozi, mtunza nyaraka mzuri na ni mwandishi.

Aidha Mzee huyo ni mkarimu, mwenye kipaji cha uongozi mtunza muda mzuri mtu wa kujituma katika kuhakikisha kama anashughulikia jambo fulani anahakikisha linafanikiwa na ni kiongozi asiyependa rushwa hata kidogo.

Lakini katika hayo niliyoyaona kwake pia nimegundua kuwa Mzee huyo bado ana maono ya kuongoza hasa katika nyadhifa za Taifa.

Na mwisho nilichobaini ni kwamba uongozi wa Mzee Mutaragara Chirangi
haukuwa katika nyanja moja tu bali ameweza kiongozi katika nyanja tofauti tofauti za elimu, kisiasa, kidini, kiutamaduni, kiuchumi na kimaendeleo.
**************************************


UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 274
JAJI, DAN P. MAPIGANO
Dar es salaam
09/09/2004

MAELEZO:

Siku ya tarehe 09.09.2004 nimefika hapa kwa kaka A. M. Chirangi kuona mradi wake Majengo ya makazi, mashamba, bustani n.k. kwa kweli ni mradi wa ubunifu mkubwa na wa kupendeza. Bila shaka utekelezaji wake kikamilifu utahitaji gharama kubwa, subira na kikubwa zaidi baraza za mbinguni. Naamini kabisa kwamba kaka ni mwenye subira, dhamira na bidii. Anachohitaji hasa ni uwezo wa kukabili gharama zinazohusika. Na kwa hilo amtegemee zaidi Mwenyezi Mungu na misaada ya hali na mali toka kwa wote wanomtakia ufanisi kidhati.

Mungu amsaidie na kumbariki.
*******************************************

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 268. Mwl. Happines Baitan & Mwl. Devotha Damas
S.L.P. 128, Musoma
Mara

MAELEZO:

SHUKRANI:
Shukurani zetu zikuendee kwa kutukaribisha nyumbani kwako na kufanya ziara kwenye nyumba yako iliyoko Kigera.

Kwa kweli tulifurahia sana ziara hiyo ya tarehe 08/05/2004, hatutaisahau maishani mwetu.

MAMBO TULIYOJIFUNZA:
Kwa kweli ni mambo mengi sana na muhimu tuliyojifunza kutoka kwa Mzee M. Chirangi, nayo ni:-

i) Ukarimu
ii) Upendo
iii) Ushirikiano na watu wa aina zote.
iv) Utunzaji wa kumbukumbu.
v) Uongozi kwa ujumla.
vi) Busara na hekima
vii) Utunzaji wa muda.

MAONI YETU:
Maoni yetu tunaomba mambo muhimu tuliyojifuza kwako mathalani ukarimu, upendo, ushirikiano, maamuzi ya busara n.k uendelee kuirithisha jamii.

Na mwisho tunakuombea Mwenyezi Mungu akujalie ili uweze kutimiza malengo yako na hasa ukamilishaji wa ujenzi wa nyumba yako ya Kigera.
Na Mungu akubariki na kukufanikisha katika yote.
***************************************************************

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 266.
MR. DAVID M. SINDA
MWENYEKITI RED-CROSS MARA 2000 - 2005
TRCS

MAELEZO:
Nimekutembelea leo tarehe 26.4.2004 baada ya kunitembeza katika miji yako, maeneo ya kazi za mikono, uandishi wa vitabu, nyaraka na utunzaji wa kumbukumbu mbalimbali.

“ NIMEGUNDUA”
Vitu vikuu vya kuigwa kutoka kwako ambavyo ni sifa za kiongozi anayefaa katika jamii.
(a) MUDA:
- Wewe unajali muda kuwa ni mali na uheshimiwe/kutukuzwa na watu wote kwani haurudi nyuma bali unaenda mbele.

(b) MCHAPAKAZI:
- Nimeamini kuwa kila mtu anatakiwa kufanya kazi kwa bidii ili uzeeni ufaidi matunda (Nyumba bora, watoto, shule).
- Umetoa nguvu zako, pesa zako, akili zako muda n.k. kwa ajili ya kuendeleza jamii ya Tanzania husasani Musoma na Kata ya Kigera (utengenezaji wa mabarabara) Mungu akubariki.
- Ni vizuri jamii iige na kutekeleza.

(c) MTU ASIYEPENDA DHULUMA:
- Mimi sikuwepo katika uongozi wako, lakini jamii inakushuhudia hukujihusisha na rushwa wala dhuluma katika jamii. Nakupongeza na Mungu aendelee kukuimarisha katika tabia hiyo.

(d) MKARIMU MPENDA ELIMU NA MTOA MISAADA KATIKA JAMII:
- Nimeangalia na kuchunguza kwa undani vitabu na kumbukumbu zako zimeonyesha umesaidia wazee, vijana, watoto katika misaada mbalimbali ya vitu, pesa, vyakula, mawazo, ushauri.
- Nakushauri usifunge milango katika talanta hiyo.
- Pia hongera kwa kusomesha watoto.

(e) KIONGOZI BORA:
- Mtafiti/mvumbuzi.
- Mwenye hekima.
- Mwadilifu na mshauri.
- Msafi. - Mpenda Mungu.

MWISHO:
Nina imani na tumaini kwa akili za binadamu kuwa wewe ni mjoli wa Mungu. Nilichojifunza kwako, Mungu akipenda nitakuwa tayari kukifanyia kazi katika jamii. Nakushukuru kunikaribisha nyumbani kwako pia kushiriki chakula cha jioni pamoja cha kimwili na kuomba pamoja kwa Mungu wetu aliye hai.
Nakutakia kazi njema na Mungu aendelee kutubariki na kutuandaa familia hizi mbili kwa WOKOVU UJAO.
********************************************

UTAMBULISHO WA MGENI:

Namba. 252.
MWL. JOHN M. SARARA.
MUSOMA TECH. SCHOOL
08/06/2003

MAELEZO:

MAONI YANGU JUU YA MZEE AMOS MUTARAGARA CHIRANGI.

Ziara yangu ya masaa 5 Nyumbani kwa Mzee A. M. Chirangi Kamnyonge na Kwangwa tarehe 08/06/2003 kuanzia saa 9 Alasiri hadi saa 2 Usiku. Ninayo mengi ya kujifunza kwetu na jamii kwa ujumla. Ilikuwa Jumapili njema.

Ni waheshimiwa wachache wanaoweza kukutana na watu wasio wa tabaka lao wakakaa kindugu, wakawapa ushauri, wakawaomba ushauri wakala na kunywa pamoja, wakaona shughuli za mfano wa kusali pamoja na hata kupoteza muda kama alivyofanya na anavyofanya Mheshimiwa Mzee Chirangi.

Ni waheshimiwa wachache wanao weza kuwaonyesha walio wengi njia sahihi ya kufuata
MUDA/RATIBA na kuonyesha kwa vitendo bila kinyongo njia ya mafanikio ikiwemo Elimu, Kazi, viwanja,Ndoa, utunzaji kumbukumbu na kuendesha michango bila kudai malipo au kamisheni.

Ni waheshimiwa wachache wanaoweza kuishi na watu bila ya kujikweza na kujivuna kwa nyadhifa zao au kikauli na badala yake kuishi na watu kuwa sehemu ya jamii.

Ni waheshimiwa wachache wanaoweza kumtukuza Mungu wakati wote wa madaraka yao na kukubalika na madhehebu yaliyo mengi.

Ni waheshimiwa wachache wanaoweza kuvumilia kuwa katika Chama cha Siasa hukuitetea Serikali ambayo inayo onyesha kuwasahau baada ya kuwa wamevitumikia vyombo hivyo kwa uaminifu, haki na uadilifu katika maisha yao yote.

Ni waheshimiwa wachache wenye kumbukumbu za kila siku za maisha yao, licha ya kuwa wanaouwezo wa wasaidizi, wanayo Elimu na vyombo vya kutunza kumbukumbu.

Ni watu wachache wenye hazina nyeti za Serikali ambazo nadhani hata Serikali inazihitaji lakini inashindwa kuzitumia.

Yako mengi lakini yote haya na sifa hizi anazo Mzee, Mwalimu A. M. Chirangi, Mwanasiasa mkongwe, Mwanahistoria, Mwandishi, Mzazi, Mzee mwenye utu, Busara na hekima anayeonekana kusahauliwa lakini HISTORIA HUENDA IKAJA KUTUSHITAKI.

Ziara yangu na maisha yake yanaelekea kufanana na ya Baba wa Taifa licha ya tofauti ya nyadhifa walizokuwa nazo. Nina imani busara na Mawaidha yake, kazi na maono yake yatakumbukwa na kudumu Daima na siku moja Mtaa, Barabara ya Chirangi itakuja kuwa maarufu si Musoma tu bali Nchi nzima.

AU.

Familia yake, watoto au wajukuu watakuja kurejesha jina na Hadhi za Chirangi kama wataenzi kazi na Busara ya Mzee A. M. Chirangi na mtaa wa Chirangi pia nyumba ya Mzee wetu iliyoko Kwangwa.

Ni namwombea Mzee Chirangi maombi yake matano yafike kwa Mwenyezi Mungu na yapate majibu mema.

Namwombea kwa Chama cha Mapinduzi na Serikali yake, vyama vya michezo, Mashirika ya Dini, Ndugu, Jamaa na Marafiki tuenzi kazi zake kufanya kila liwezekanalo kuenzi kazi zake na busara yake na kujibu maombi yake kwa vitendo.

Aidha namwombea Mzee M. Chirangi asijutie aliyoyafanya na matusi au bezo anazozipata. Hata Yesu alitemewa mate leo tunamtukuza. Farijika na kuwa na familia yenye furaha, iliyoelimika na matunda ya kazi zako na misaada uliyotoa Mungu akubariki na atakupa afya njema.

Tuombee na sisi tunaothamini mchango wako wa hali na mali na busara zako zimekuwa kioo na dira kwetu, WASAMEHE WALIOKUKOSEA.
Na siku Mungu akikuchukua usijutie, farijika kwa vile umejiandalia kaburi na staili ya mazishi ulale pema peponi, uiombee Musoma, Tanzania na Dunia kwa mema.

Ziara yangu kwako ni ya KIHISTORIA, KIOO NA DIRA, nitakuja tena kuchuma Busara zako.
*************************************************************************

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 242.
Lucas O. Wadenya
S.L.P 1405
Kisumu - Kenya -
03 Octoba 2002

MAELEZO:

Mimi Lucas O. Wadenya nimemtembelea Ndg. Mutaragara Amos Chirangi na kutembezwa katika mazingira yake yote. Mambo ambayo nimevutiwa na Mzee huyu ni mtunzaji wa takwimu zote za kila siku za aina zote kitu ambacho sijawahi pata kuona kwa mtu yeyote tangu niwepo. Pia ameteyalisha kaburi hivyo amekumbuka kuwa kuna kifo kitu ambacho si rahisi kwa watu wengi. Molla akuzidishie baraka.
***********************************************************************************
UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 194.

Ndg. C. I. Mtengera,
MHASIBU HAZINA NDOGO
MKOA WA MARA
S.L.P. 974,
Musoma
October, 1999

MAELEZO:
Mpendwa Mzee A. M. Chirangi,

Nashukuru kwa kunipa fursa ya kuyatembelea maeneo ya KIGERA na KWANGWA ambayo kwa juhudi zako binafsi ukiwa kiongozi wa Chama uliwezesha maneno hayo kupimwa na barabara nyingi kupasuliwa.

Ni kitendo cha kuruhusu watu wa kawaida na wa juu kufika na kutembelea nyumba yako ni ushahidi sahihi kuwa nyumba hiyo haukujenga kwa kipato chenye hila.

Hivyo nakuombea kwa Mungu akujalie maisha mema uweze kukamilisha jengo hilo.
Kadhalika namwomba Mungu azifungue nyoyo za watu waweze kukubali kutoa michango yao ya hali na mali uweze kulikamilisha jengo hilo na hatimaye uhamie na kuishi humo. Hivyo ndivyo njia pekee ya kukuenzi na kuzikumbuka fadhila zako kwa wananchi.

IKUMBUKWE KWAMBA KILA MTENDA WEMA DAIMA ATAKUMBUKWA KWA WEMA.
********************************************************


UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba.157.
B.M. MAZIKU
MHANDISI WA MJI, MUSOMA.

MAELEZO:

Nimetembelea eneo la Mzee A. Mutaragara anakojenga nyumba mpya. Nampongeza sana kwa juhudi zake hizo. Pamoja na yeye kujitolea kutengeneza Barabara.

UTAMBULISHO WA MGENI:
Namba. 209.
Ng’araga
AFISA UHUSIANO
VI- Agroforestry Mara
20/01/2001

MAELEZO:
VI – Agroforest Project inampongeza Mzee A. M. Chirangi kwa ujumla kwa yote ambayo yanaendelea katika eneo lake. Hii ina maana kwamba yeye ni kielelezo bora ndani ya Mji wa Musoma.

Katika matendo yake na utekelezaji wake Mutaragara mradi tutakuwa naye katika kuboresha mazingira ya kilimo mseto katika maendeleo yake. Pia shamba hilo litakuwa ni mfano kwa watu wa Kata ya Kigera.

Namtakia kazi njema na Mwenyezi Mungu amsaidie.











Nyote bado mnaendelea kukaribishwa. Baada ya utafiti na mashauriano kuhusu hiyo nyumba iliyoko eneo la Kwanga, mipango imewekwa kuwa siku za usoni ukifuata hicho kibao cha Chirangi Street utakuta na Bethsaida Centre for Health and Development ambapo huduma mbalimbali za Afya zitatolewa kwa wananchi ikiwa ni sehemu ya kumuenzi Baba katika harakati zake za kunyanyua viwango vya maisha ya Watu.
____________________________________
----------------------------------------------------------------

1 comment:

Anonymous said...

Du baba baba !!kweli sasa nazidi kumfahamu zaidi huyu mzee alivyoluwa mtu wa watu na maendeleo.
Mungu ailaze pema roho yake.

mwana ukwata