Thursday, January 3, 2008

VIUMBE SABA , IMANI JUU YAO NA MATUMIZI YAKE KWA WATU WA JAMII YA WARURI NA MAKABILA YANAYOLANDANA NAO KATIKA UKANDA WA ZIWA VICTORIA.








Hii ni moja ya Makala nyingi zilizoandikwa na Mutaragara Chirangi.

Jamii ya Waruri na makabila yanayoshabihiana kwa karibu kiutamaduni kama vile Wakwaya na Wajita wamekuwa na imani mbalimbali juu ya baadhi wa wanyama wa aina mbalimbali. Aidha wamewatumia wanyama hao katika maisha yao ya kila siku si kwa ajili ya chakula bali zaidi kama nyenzo katika tiba au kuboresha shughuli za maisha yao. Hapa chini nakutajia viumbe saba na matumizi yao.

I. INDURUTI
Induruti ni jamii ya wadudu wadogo kama Inzi mdogo.
Kuna aina mbili za Induruti kama ifuatavyo:-
A. Iduruti inayozalia ndani ya mashimo ya miti na mapango ya mawe.
B. Induruti inayozalia katika mashimo ardhini.

Uwezo / Matumizi
Induruti ni miongoni mwa viumbe wenye sifa kubwa. Waganga wa Tiba Asilia hutambua umuhimu wao na kuwathamini. Matumizi mengine ni kama vile ifuatavyo:-

A. Induruti inatoa asali nzuri na tamu kuliko asali ya nyuki ambayo hutumika kama chakula na wengine kuitumia kama sehemu ya dawa asilia, kama dawa kuongeza mvuto wa kimapenzi, kama dawa kwa ajili ya biashara,kama dawa ya kuzindua miji ya watu, dawa kwa ajili ya ushindi wa michezo n.k
B. Induruti huaminika kuleta taarifa mbalimbali kwa kuandamana na watu njiani kama askari ili kufuchua ‘siri’ za watu.


II. IMBURUKAKA – (Kaka-kuona)
Imburukaka ni jamii ya keng na kobe na pia hujongelea polepole. Ingawa ni mkubwa kuliko kobe, Imburukaka ni kudra sana kuonekana kwa watu. Mahali alipo mara nyingi unaweza kukuta pia wanaishi na nyoka wa eneo hilo. Imburukaka ina uwezo wa kuvuta viumbe vingine.

Uwezo / Matumizi
Waganga wa Tiba Asilia wanaitumia kwa dawa ya:-
A. Mvuto kwa watu - Ekisagara
B. Kuongeza mauzo katika Biashara – Samba
C. Hutumika kwa Mazindiko ya miji na kwa kinga ya watu.
D. Huweka hofu – mamlaka ya utawala uwezo kama Simba.
E. Samba ya mapenzi na zindiko.


III. INJILILI (NYAMWERA OMWANA WA INJILILI)
Injilili ni ndege mwenye umbo zuri la kupendeza na kuvutia. Katika macho yake, Injilili ana ngozi au utando wa aina mbili, unaomuwezesha kuona ndani ya maji na wa pili humuwezesha kutumia katika nchi kavu, kama mamba. Injilili ana manyoya mazuri sana na hayalowani maji kwa urahisi kama ya bata. Ana manyoya yenye rangi zaidi ya tatu – udhurungi, Kijani, nyekundu, bluu na nyeupeInjilili ni aina ya ndege mwenye hulka na uwezo mkubwa kwa kujitosa kilindini (Murwena kuruondo) na kutandika kiota cha makazi yake huko kwa kuzificha siri zake ndani sana

Majina mengine ya Injilili.
Anaitwa Injilili Nyamwalika kuruondo – kurwena mwitubi bhya magoji (Kilindini). Pia anajulikana kama Injilili mzalia chini ya Bahari kama alivyo Mzamia lulu madini yenye thamani kubwa

Uwezo / Matumizi
Waganga wa Tiba Asilia uthamini viungo vya ndege huyu kwa ajili ya matumizi ya dawa hususani kama vile:-
A. Dawa ya mvuto – (Samba)
B. Kuzuia bahati mbaya (nuksi)
C. Kuepusha madhara au maafa fulani



IV. OMUNYAMUNYA.
Omunyamunya ni jamii ya mnyama mdogo sana kama panya mkubwa (panya- buku). Ngozi yake ina mfano wa miiba kama ya Nungunungu.

Uwezo / Matumizi yake
A. Hutumika kuongeza mvuto wa mapenzi na wa biashara
B. Hutumika kwa kuweka zindiko la mali



V. IPINGU.
Ipingu pia ni jamii ya ndege mdogo.

Uwezo wake
A. Ana uwezo mkubwa wa hurka ya maono na hisia.
B. Ana uwezo wa kutambua ni wapi kuna mzoga hata kama ni mbali kwa kutumia milango yake ya fahamu kama Fisi.
C. Kusaidia kugundua mazuri na mabaya.

Matumizi yake
A. kusaidia Kutambua mazingira ya mahali fulani
B.Kusaidia kutambua maadui walipo.
C. kuongeza uwezo wa kutambua na kutafsiri ndoto ( imbwira)

VI. KUNJU MUROGOMBI:
Kunju ni jamii ya ndege. Kunju anaumbo la mvuto. Ni msafi na muimbaji hodari kwa kuigiza semi au sauti za watu.

Uwezo / matumizi yake.
A. Hutumika kama pambo
B. Jina lale (Murogombi) hutumiwa na wanasiasa kumtambulisha Mhutubu shupavu



VII. ITARITA – MUFUBYA NG’ENDO (SAFARI)
Itarita ni jamii ya ndege akaaye porini kwenye miti na mapango ya mawe. Ni ndege aliyefunikwa na manyoya mengi.

Matumizi yake
kitokea ndege huyu akalia wakati mtu anaandaa safari (Orugendo), basi mtu huyo huweza kuahirisha hiyo safari. Safari huahirishwa pia pale ambapo ndege huyu anapokatiza barabara/njia mbele ya mtu aanzaye safari. Imani ni kuwa safari hiyo itakuwa na mikosi au matatizo fulani makubwa. Ndiyo sababu anaitwa Mukubya – Mufubya Ng’endo yaani Mvunja safari.

Hivyo Itarita hutoa tahadhari kwa wasafiri na hivyo pia kuaminika kuwa mpiga mbiu ya taadhari wakati wa hatari.

2 comments:

Anonymous said...

hii ni kali sana familia iombwe iwaazime watu wa makumbusho ya Taifa maana nina amini hakuna maelezo ya hivyo juu wa watu wa mkoa wa Mara huko.

malima said...

Hii iwekwe kwenye wikipedia tafadhali. Du mzee chirangi hakuwa wa mchezo!