Monday, September 20, 2010

Matumizi Holela ya Msimu 'Chakachua'




Utangulizi
 Chakachuliwa,  ni msamiati nyumbulifu (derivative word) toka neno mzizi chakachua  uliotumika katika mijadala Bungeni na sasa pia waandishi wa habari kueleza hali ya mafuta (dizeli & petroli) yaliyochanganywa na vimiminika vingine kama vile mafuta ya taa, maji n.k ili kuongeza ujazo kwa ajili ya kujipatia faida zaidi baada ya mauzo (kwa bei ile ile) ya bidhaa hiyo iliyoteremshwa thamani ulinganisha na uhalisia wake.
 Sina hakika kama neno hili linatambuliwa rasmi na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) ambalo kisheria ndilo lenye mamlaka ya kuratibu shughuli za uundaji wa istilahi za Kiswahili. Wala si yakini kama utafiti wa kina umefanywa na Taasisi yeyote yenye ithibati kama vile TUKI juu ufafanuzi wa dhana iliyobebwa katika istlahi hii kutoka lugha chanzi na hatimaye uundaji wa kisawe hicho cha chakachua.  Mpaka hapo itakapoelimishwa vinginevyo, neno hili nalichikulia kama kisawe kisicho rasmi katika lugha ya Kiswahili.


Eneo Stahiki Kiteminografia
Kwa kuzingatia mbinu ya kiteminografia (terminography), hili neno chakachua linastahili zaidi  kuonekana katika Kamusi ya Istilahi ya Sayansi-Fani ya Kemia hususani kwenye somo la taitresheni (titration) ambapo kuna uchambuzi wa matokeo ya uchanganyaji wa vimiminika tofauti sanjali na udhibiti wa ujazo wake.
 Maana & Kusudi
Kuchakachua  ni udanganyifu kwa kusudi la ama ki- biashara katika kutafuta faida kubwa kwa njia isiyo halali au kwenye upimaji (tests) ambapo matokeo fulani yanalazimishwa ama yaonekane au yasionekane kinyume na hali halisi. Mara nyingi kuna njia kuu tatu za udanganyifu katika vimiminika kama vile:-
 1.      Adulteration –  ughushi kwa kuongeza vimininika au kuchanganya na vitendanishi  (reagents) duni
2.      Dilution   - uchujuaji kwa kuongeza zaidi maji
3.      Substitution – kibadala, kwa kuongeza kimiminika mbadala.   

Matumizi ya neno
Pamoja na changamoto katika lugha yetu ya Kiswahili ya kuwa na upungufu wa istilahi anuwai katika uwanja wa Sayansi na Teknolojia, hivi  karibuni, neno kuchakachuliwa  limetumika kama msimu katika medani za siasa na kijamii kwa ujumla katika tamathali za semi na kwa mapana kama sinonimi (synonym) ambapo  istilahi moja ya Kiswahili inahusishwa na dhana zaidi ya moja katika lugha chanzi. Ndiposa neno hili limeweza kutumika kubeba dhana kadha wa kadha hadi kuleta mikanganyiko, kama vile kughushi, kubadilisha, kutotenda haki, kuharibika, kudanganya, kubatilishwa (mfano, leo nimesikia mtangazaji akisema kuwa “Ratiba ya ligi kuu imechakachuliwa”) n.k,  na hata –enye utata,  (mfano mtu anasema, “Alipata mchumba aliyechakachulika”akimaanisha mchumba mwenye utambulisho tata) n.k
 
Pendekezo
Ningekuwa na uwezo wa kushawishi BAKITA, ningependekeza kuwa kisawe rasmi kinacholandana na dhana nzima ya kupunguza uthamani wa kimiminika kwa kuchanganya na kitu kingine kiwe  kuchukuchua  badala ya kuchakachua. Kwamba neno mzizi liwe chukuchua ambalo linaweza kutoholewa kutoka chukuchuku mf. mchuzi chukuchuku  ambao ni mchuzi mwepesi usio na thamani inayoridhisha, mchuzi uliowekwa maji mengi (omusosi omujubhe) kupita kiwango kitakiwacho  hivyo mafuta yaliyochukuchuliwa ni mafuta yasiyo katika kiwango kitakiwacho ni mafuta yaliyoonhezwa kimiminika kingine na kushusha ubora wake.
  
Nathubutu kusema,


Musuto wa- Mutaragara wa- Chirangi




Verbal Diarrhoea Dehydrates Human Dignity. Chirangi, (2000)



(Shukrani kwa Blogu ya barclayp yenye picha)

Thursday, September 16, 2010

TUPULIZE VUVUZELA

Video: Vijanazaidi -You Tube. Shukrani kwa Kikwete 2010 Campaign Team & Michuzi:


Tanbihi: Nisemalo hapa laweza lisiwafurahishe wengine lakini linabaki kuwa kweli:

  • SANAA ILIYOUNDWA INA WELEDI WA HALI YA JUU . 
  • MAVAZI YALIYOTUMIKA NI YA HESHIMA NA YAMELANDANA NA JAMII (WANA CCM) HUSIKA PAMOJA NA SHUGHULI ILIYOPO
  • STAILI MPYA ILIYOONESHWA (KIDUKU) IMEKONGA NYOYO
  • MATUMIZI YA VUVUZELA NA RANGI ZAKE YANANYANYUA HISIA ZA MWAFRIKA KATIKA SHUGHULI ILIYOFANA HUKO BONDENI
  • MELODI YA MARLAW KAMWE HAISHAWISHI HASIRA BALI UTULIVU, MBEMBELEZO NA MGUSO WA MWILI NA ROHO
  • UCHAGUZI WA MANENO KATIKA WIMBO UNAHAMASISHA WANACHAMA NA PIA UNATUMA CHANGAMOTO KWA WANACHAMA WA VYAMA VINGINE
  • USHIRIKI WA  NGUVU WA VIJANA KWA HIYARI NA MUZIKI WA KISASA TANZANIA NI UBUNIFU NA FURSA ILIYOTUMIKA NA TIMU YA KAMPENI KWA UMAKINI KATIKA KARNE YA LEO!

WAHUSIKA WOTE WANASTAHILI PONGEZI!

NINACHOWEZA KUSHAURI TU NI KUWA,
NAFASI YA MADANSA WA KIKE INGEWEZA KUBORESHWA KWA KUWAPA MUDA WA UWIANO NA WALE WA KIUME JUKWAANI.

Saturday, August 21, 2010

WOSIA KWA WAHITIMU WA 2010 KISARE NURSING SCHOOL

Vitabu katika Maktaba ya Kisare Nursing School
Wapendwa Wahitimu,
Kisare Nursing School,
Mugumu, Serengerti,

Sanjari na kuwatunuku Wahitimu vyeti husika, mara nyingi inapofika siku ya mahafali mengi yanasemwa na kuimbwa katika ama kuwapongeza au kuwahasa kama siyo kuwaangaliza katika majukumu yatakayowakabili katika jamii.

Turuhusuni nasi leo tuwatunuku nukuu chache zinazohusika na KUPATA ELIMU kama tafakuri mtakazozibeba katika fikra zenu kama zilivyoanikwa na magwiji katika nyanja na tasnia mbalimbali kama ifuatavyo:-

 “Vitabu vyaweza kuwa hatari, vile vyenye uzuri wa hali ya juu, ni vema vikawekewa tahadhari isemayo, Onyo, hiki kinaweza kubadilisha maisha yako”. Helen Exley .


 “Vitabu na maandiko yote ni tishio kwa wale wanaonuia kuiminya kweli.”
Wole Soyinka.


 “Upo utofauti kati ya mwenye ari atafutaye kusoma kitabu na asiye na ari atafutaye kitabu cha kusoma”. Gilbert Chesterton


 “Kusoma ni nauli yenye unafuu kuelekea kokote”. Mary Schmich.


 “Elimu yetu inatakiwa kutupa chanjo ya kujituma kwa ajili ya jamii nzima na kuwasaidia wanafunzi kukubali yale yanayokubalika kwa ajili ya maisha yetu ya mbeleni”. Baba wa Taifa, Mwl. J. K. Nyerere


 “Elimu ni siraha ya nguvu kubwa unayoweza kutumia kuibadili dunia”. Nelson Mandela.


 “Mizizi ya elimu ni michungu, lakini matunda yake ni matamu”. Aristotle.


 “Wakati mnaondoka hapa (Chuoni), msisahau kwa nini mlikuja hapa”. Adlai Stevenson








Masomo yenu hapa yanaweza kuwa yamefika ukingoni,
lakini kumbukeni kuwa kuelimika kunaendelea daima!
Wahitimu, Wakufunzi, Watumishi na Wadau wengine wote
hongereni sana na tunawatakieni kila la kheri.


Wenu,

Judy, Marja & Musuto Chirangi
Uholanzi, July, 2010.

Friday, August 20, 2010

MFANO WA MWANA DIASPORA SHUJAA

“…Why should my face not look sad when the city where my fathers are buried lies in ruins, and its gates have been destroyed by fire?" Nehemiah 2:3

MISINGI 10 ALIZOTUMIA MWANA DIASPORA SHUJAA


1. Kuwa na mawasiliano endelevu na nyumbani kujua si tu habari za kifamilia lakini pia maisha ya jamii na maendeleo yao kwa ujumla.
2. Kuwa na mzigo na matatizo yaliyoko nyumbani.
3. Kumshirikisha Mola katika mipango na mafanikio yetu.
4. Kutumia fursa na rasilimali tulizo nazo kwa ajili ya maendeleo ya jamii yetu
5. Kufanya tathinini za kisayansi za matatizo / mahitaji yetu halisi na kuweka mipango kazi na mikakati.
6. Kuhamasisha wengine na kugawana majukumu ikiwezekana kwa kujali vipaji / uzoefu / uwezo wetu.
7. Kushiriana pamoja kutekeleza mipango kazi.
8. Kutokuyumbishwa wala kukatishwa tamaa na wanaotubeza na au wanaotaka kutuondoa katika maono na mwelekeo wetu wa ki-maendeleo.
9. Kuonyesha ushujaa, kujilinda na ikibidi kupambana na wale wanaotaka vita na sisi.
10. Kusimamia haki, maadili na kuwajali wahitaji zaidi.

Kanuni hizi nimezinyambulisha nilipomkumbuka Kiongozi - shujaa mmoja katika Agano la kale, aliyeitwa Nehemia.

TAFADHALI KAMA HUJAWAHI SOMA AU KUTAFAKARI KWA UNDANI KITABU CHA NEHEMIA WAKATI NDIO SASA!
N.B Hata katika misaafu mingine kama Koran na hali kadhalika Hadith kuna mashujaa na wanamapinduzi wengi tu kama Nehemia.

Kwa kifupi tu ili kukupa hamu ya kusoma,

 Nehemia alikuwa mshika kombe (the Cup- bearer) wa Mfalme wa Uajemi. Pamoja na kuwa katika maisha mazuri huko ughaibuni na katika hiyo kazi ya watu wachache sana katika ‘special branch’, katika kuwasiliana kwake na nyumbani, alipata habari kuwa kuta za Yerusalemu & malango yake vimebomolewa na kuchomwa moto.
 Alibeba mzigo wa taabu zilizokuwa zinawakabili watu wa nyumbani Jerusalem, akahuzunika na kuomboleza sana.
 Akamwomba Mola juu ya jambo hilo
 Akatumia nafasi yake kumwendea Mfalme ambaye alimpa ruhusa na kumpa usalamana pia vitendea kazi vya kuanzia kazi ya ujenzi. (Sisi tunatumiaje vipawa na nafasi tulizo nazo kuendeleza jamii zetu?)
 Alipofika kabla ya kuanza kazi alifanya tathmini ya kiwango cha uharibifu na kazi iliyotakiwa kufanywa na kupanga kazi.
 Akahamasisha wenzake na kuwaambia kuwa tujenge pamoja, kazi iligawanywa vyema kufuata uzoefu/ uwezo. Mfano Makuhani walipewa kushughulia mlango waliouzoea na kuufahamu – mlango wa kondoo!
 Watu walishirikiana wakachapa kazi mchana na usiku
 Kuliibuka akina Sanbalati, Tobian na wenzao wakawabeza na kutaka kuwaondoa kazini, lakini Nehemia alisisitiza kuwa hawezi kuacha kazi.
 Maadui walipopanga njama, ulinzi mkali uliwekwa na wakapambana nao. (Ni aibu sisi leo tunakatishwa tamaa wala hatupambani na maadui wetu katika maendeleo!)
 Nehemia aliwasimamia haki kama kuwasaidia maskini n.k na pia akawawajibisha wakiukaji ili kulinda maadili yaliyokubalika.

Hitimisho:


Yawezekana tukawa na maisha bora zaidi popote tulipo nje ya mji au nchi, inatubidi kubeba mzigo na kuhuzunika na hali yoyote mbaya (kama ipo) katika jamii zetu. Mbele ya Viongozi wetu au Mashirika yenye uwezo au yeyote mwenye uwezo wa kutusaidia kutatua tatizo lililopo, tunapaswa kusema kuwa,
“Tutakosaje kuwa na huzuni wakati mji/ nchi ya baba zetu na mama zetu ina hali isiyoridhisha?”
Halafu tufanye kweli kwa tuchukuwa hatua 10 za kuleta maendeleo kama kiongozi wa mfano Nehemia alivyofanya.

Verbal Diarrhoea Dehydrates Human Dignity. Chirangi (2000).

Tuesday, August 3, 2010

UGONJWA WA TAFSIRI NJE YA MAZINGIRA (Contextomy)


 Zao la Sanaa hiyo hapo juu ni vazi-potosha liloundwa nami mwenyewe kuonyesha jinsi ugonjwa nyemelezi wa Tafsiri nje ya mazingira yake (Contextomy) unavyoweza kuwa na athari katika kupotosha umma. 

Pata chanjo yake mapema kwa kutafakari jambo katika mazingira yake na katika ukamilifu wake!

Tuesday, July 20, 2010

Wahubiri katika sauti zenye Mpangilio

Kwanza Bofya kwenye play button ya Redio hapa chini usikilize.




Miziki ya kumsifu na kumtangaza Mungu imekuwepo tangu enzi za agano la kale na inaendelea kukua kwa kasi katika mapigo,ghani na staili kadha wa kadha za uchezaji wa Waimbaji.

Umuhimu wa nafasi ya muziki katika Makanisa, Misikiti na Masinagogi ni mkubwa sana katika kusaidiana na Wahubiri wengine kufikisha ujumbe kwa hadhira inayokusudiwa.

Aidha Kwaya ziimbazo au zipigazo miziki ya Kiroho pia kama  walivyo mawakala wengine wa mabadiliko ya mwanadamu, zimefanya kazi kubwa ya kuwabadili, kuwafariji, kuwahubiri, kuwashawishi,  kuwafundisha, kuwaonya na hata kuwapagaisha wanadamu wengi, mimi nikiwa mmoja wao!

Ukiachilia wasanii au kwaya ambazo zimeshapiga hatua kubwa, Wahubiri hawa wa sauti zenye mpangilio wanakabiliwa na changamoto nyingi, hapa chini leo nataja mbili tu:- 

1. Kuhakikisha kuwa ujumbe wao unahaririwa na kupangwa vyema kabla haujawafikia hadhira. (si kujali tu mipangilio ya midundo na staili za kuruka)

2. Kurekodi kazi zao na kuwa na hati miliki. Wengi wametunga nyimbo na baada ya muda zimeachwa na kupotea tu bila kutunzwa, hapa namkumbuka Mwalimu wangu Julius Zabuloni Machumu (RIP), ambaye hadi mauti yake hakuwahi kurekodi kazi yake ya usanii iliyokuwa na ubunifu wa hali ya juu enzi hizo za miaka ya 80. Kati ya vibao vyake vilivyotikisa katika makambi ya kiroho ni  Katondo tondo Maryamu Nemuka, Isaka, Kinachoshangaza, Jerusalem, Paliondokea Yohana Mbatizaji n.k 

Wito:
Wadau wote tujifunge vibwebwe kuwasaidia Wahubiri hawa kwa kadiri ya uwezo wetu na vipawa vyetu  maana utume wao na jumbe zao ni za muhimu sana katika maisha yetu leo na kwa vizazi vijavyo.


Hapa chini ni picha ya Mwalimu mzoefu wa Kwaya ya Upendo ya Kanisa la Mennonite Tanzania Mugumu,  ndg. Gemma Igira (mwenye shati nyeupe) akiwa na Mwalimu mwenzake gwiji katika muziki wa injili ndani ya Studio yenye wapishi wa muziki waliobobea ijulikanayo kama Studio Habari Maalum  Mwanza wakati waliporekodi Album ya Upendo Choir kwa jina la Tenda Miujiza. Heshima kuu kwa Waalimu wote waliotoa msaada mkubwa, Wanakwaya wote walioshiriki kutoka Jimboni kwao chini ya uongozi wa jimbo wa Mchungaji  Wilson Shanyangi Machota.  .

Ukipenda kujipatia nakala yako ya Album hiyo ambapo kibao hicho hapo juu (SIFUNI) kimo ndani wasiliana moja kwa moja na Uongozi wa Kwaya ya Upendo au Uongozi wa Jimbo (KMT- Mugumu c/o S.L.P 17 Mugumu, Serengeti, Tanzania au tuma barua pepe kwa gemma.igira@hotmail.com.